Thursday, October 15, 2015

HASIRA HASARA PIA NI MBAYA KWA AFYA ZETU!!!

Sisi sote hukasirika mara kwa mara. Hasira ni sehemu ya hisia zetu kama vile ilivyo upendo, tumaini, wasiwasi, huzuni na woga. Hasira ilivyodhibitiwa inaweza kuonyeshwa kwa njia inayofaa na inaweza kuwa na faida. Kwa mfano, hasira inaweza kuwa na faida ikiwa itamfanya mtu aazimie kushinda vizuizi au matatizo fulani.

Kwa kawaida, mtu huudhika anapotendewa isivyo haki. Kutukanwa, au kukosewa heshima kunaweza pia kumuudhi mtu. Pia, mtu anaweza kuwa na hasira anapoona jambo fulani kuwa tishio kwa mamlaka au sifa yake.

Bila shaka, watu hukasirika na mambo tofauti ikitegemea umri, jinsia, na hata utamaduni wao. Isitoshe, watu hutenda kwa njia tofauti tofauti wanapopandwa na hasira. Watu fulani hawakasiriki upesi, nao husahau haraka wanapokosewa, lakini wengine hukasirika kwa haraka na huenda wakaendelea kuwa na hasira kwa siku nyingi, majuma , miezi au hata miaka.

Binadamu tumezungukwa na mambo yanayoweza kuchochea hasira. Zaidi ya hilo, siku hizi watu wanachokozeka kwa urahisi zaidi, Kwa nini imekuwa hivi? Sababu moja ni kwamba kuna mtazamo wa ubinafsi  yaani umimi ambao umeenea mno.

Kwa kweli, watu wenye ubinafsi wasipopata kile wakitakacho, mara nyingi wao hukasirika. Kuna sababu nyingi kwa nini mwelekeo wa watu kulipuka kwa hasira unaongezeka, ambazo wewe msomaji na mimi twaweza kusaidiana kuzifikiria...

Na kama tunavyoelewa hasira imekuwa ni adui kwa watu wengi sana kwasababu imekwisha leta madhara makubwa sana kwa wengi
Binadamu anadaiwa kuwa ni kiumbe ambaye anakabiliwa na tishio la kuangamia kwa hasira kwasababu ya maendeleo anayoyafikia
Hivi ni kweli  kwamba kadiri maendeleo yanavyoongezeka ndivyo uwezekano wa binadamu kuwa na hasira unaongezeka pia?.Kama ni kweli ipo hivi,  kwa binadamu  ni kitisho kwa usalama wake mwenyewe
Kuna haja ya kuwa na elimu na semina kwa wingi ili kuweza kumuokoa binadamu na kitisho cha hasira

2 comments:

ray njau said...

“Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako, maana hasira hukaa kifuani mwa mpumbavu”

Tunayo kila sababu ya kumshukuru Mungu,kwa pumzi na uhai aliotupa.
Mwanadamu yeyote aliyeumbwa na Mwenyezi Mungu ana hisia mbalimbali ambazo humfanya kuwa hivyo alivyo. Mojawapo ya hisia hizo ni hasira. Lakini ni vema kujitambua na kuitawala hasira yako kabla haijakutawala.

Hivyo basi, kama hupatwi na hasira, ni lazima utakuwa na tatizo. Pia ni vema kutambua kuwa kupatwa na hasira ni hali ya kawaida. Ni suala la hisia za muhimu kwa afya yako. Tatizo linakuwepo ,ni pale mtu anaposhindwa kuzuia hasira yake na kuchukua hatua na kuanza kupigana au kugombana na watu pasipo sababu ya msingi.

Hasira isiyo na mipaka inasababisha vurugu zinazoleta uharibifu. Ni sawa na ugonjwa, usipoizuia hasira inaweza kukudhuru na kukukereketa moyoni kwa njia ya fundo, husuda, chuki.
Wakati haya yanatokea, njia pekee ya kuondoa hasira ni msamaha. Kuwa tayari kusamehe na kusahau. Safisha akili na moyo wako. Rudisha chuki kwenye upendo.

Unaporuhusu furaha moyoni mwako unapata afya. Kwa kuwa inakufanya uwe huru na afya bora. Watu wenye furaha wana afya na watu wenye afya wana furaha.
Vile vile, kicheko ni dawa kubwa, Pia ni afya. Inaondoa hali ya kukata tamaa. Madaktari wanasema kicheko,ndiyo dawa pekee ya dunia. Kicheko hukuletea furaha, amani na utulivu katika akili yako na mwili.

Unaweza kuepuka magonjwa ya akili kwa kujifunza kuwa na furaha pamoja na kucheka.
Pia jambo lingine la kuzingatia, ni kwamba usile chakula wakati una hasira, vinginevyo hakitafanya kazi mwilini au kitakusababishia vidonda vya tumbo.
Ni desturi kwamba, kabla hujakaa na kuanza kula unanawa mikono, vile vile ni vema kusafisha akili yako na kuondoa hasira uliyokuwa nayo, uchungu, uhasama na mawazo mabaya. Endapo unakula ukiwa na hisia hizo, chakula unachokula kinakuwa hakina ladha, pia hakitaweza kufanya kazi vizuri mwilini.


Ni jinsi gani unaweza kuzuia vidonda vya tumbo visikupate,kwasababu ya hasira?

“Busara ya mtu huiahirisha hasira yake; nayo ni fahari ya kusamehe makosa”

Kwanza utambue kuwa vidonda vya tumbo mara nyingi husababishwa na wasiwasi, hasira, uchungu, uchovu na utumiaji wa sigara pamoja na vinywaji vikali.
Kamwe usiache matatizo yako yakakuzidi, yaachilie kwa kuzungumza na watu unaofikiri kuwa wanaweza kukusaidia. Wakati unapojisikia vibaya, jisogeze taratibu baada ya kuacha kile ulichokuwa ukikifanya ili upate muda wa kupumzika,kumuomba Mungu au hata kulisoma neno takatifu litakutia moyo.
Punguza matatizo yako kwa kujishughulisha,kwa kazi tofauti tofauti,usikae bure mawazo yatazidi kukusonga.. Kama utapenda kuwa na furaha na amani moyoni mwako itakufanya usipate vidonda vya tumbo. Kumbuka hali ya furaha ya mara kwa mara inakuondolea hali uliyonayo ya huzuni, majonzi au hasira na kukufanya uwe na afya bora.
Njia nyingine inayoweza kukufanya uepuke kupata maradhi ya moyo ni kuondoa wasiwasi na kula vyakula ambavyo havina mafuta mengi. Wataalamu wa afya wanaamini kuwa maradhi ya moyo yanaweza kuzuilika kuanzia kipindi cha ujana.
Pia wanaamini kuwa vyakula vya mafuta, shinikizo la damu, kukosa mazoezi, hasira, ulevi, msongo wa mawazo na uchovu unasababisha ugonjwa huo.
Ili kujiepusha ni vema kupata muda mzuri wa kupumzika, zuia hasira,kufanya mazoezi, kuondoa hofu, kutokuvuta sigara, kutokunywa pombe, jitahidi kutokuwa na uzito utakaozidi pamoja na kuangalia afya yako mara kwa mara.

Usirudishe hasira kwa mtu ambaye amekutenda uovu. “Watu wasiolipa baya kwa baya, au laumu kwa laumu; bali wenye kubariki kwa sababu hiyo ndiyo mliyoitwa ili mrithi baraka.”

Hasira huleta ugomvi, rafiki tafakari haya : “Kwa maana kupiga maziwa huleta siagi; Nakupiga pua huleta damu; kathalika kuchoshea hasira hutokeza ugomvi.”

Mungu akusaidie unapochukua hatua yakusamehe na kusahau,ili usije ukapatwa na ungonjwa kwa sababu ya chuki. Asante!(pendajirani.com)

Yasinta Ngonyani said...

Kaka Ray ulichosema ni kweli kabisa...Ahsante kwa mchango wako.