Wednesday, February 25, 2015

MTWA MPYA WA WAHEHE NA HISTORIA YA MAREHEMU ABDUL MKWAWA

 


Adam Abdul Sapi (13) ametawazwa kuwa Chifu mpya wa Wahehe, akirithi nafasi ya baba yake, Abdul Sapi Mkwawa (66) aliyefariki Februari 14, 2015 na kuzikwa katika kijiji cha Kalenga, nje kidogo ya mji wa Iringa ndani ya makumbusho yaliyowekwa fuvu la babu yake, Chifu Mkwavinyika Munyigumba Mwamuyinga Mkwawa.
Kabla ya kifo chake kilichosababishwa na maradhi ya sukari na figo, Abdul Sapi Mkwawa aliyekuwa mtoto wa tatu wa Spika wa kwanza mweusi nchini, Adam Sapi Mkwawa, alikuwa akifanyakazi katika kiwanda cha maji Afrika cha Kidamali, Iringa.
Amewahi pia kufanyakazi katika Chama cha Wazalishaji Tumbaku Iringa na Shirika la Elimu Supplies.
Alizaliwa Mei 4, 1949 katika kijiji cha Kalenga na kupata elimu ya msingi katika shule za Kalenga na Tosamaganga kati ya mwaka 1956 na 1963.
Mwaka 1964 hadi 1970 alijiunga na shule ya sekondari Iyunga na Mkwawa, ambako alipata elimu ya kawaida na ya juu ya sekondari kabla ya kujiunga na elimu ya juu ya biashara na utawala 1971 hadi 1973.
Mmoja wa ndugu wa marehemu, Hussein Sapi alisema mpaka umauti unamkuta, Abdul Sapi Mkwawa alikuwa Mtwa (Chifu); alisimikwa mwaka 1999 baada ya kifo cha baba yake, Adam Sapi Mkwawa aliyefariki Juni 25, 1999.
Kabla ya maziko ya Chifu huyo, wazee wa kabila la Wahehe walimsimika Adam ambaye ni mtoto wake wa tano, kuwa Chifu mpya wa kabila hilo.
Hata hivyo, mtoto huyo aliyeko darasa la Saba katika shule ya msingi ya Highlands ya mjini Iringa, atalazimika kusubiri kufanya shughuli za kichifu mpaka atakapotimiza umri wa miaka 20. Badala yake, mdogo wa marehemu, Saleh ndiye atakayeshikilia wadhifa huo mpaka Adam atakapofikisha umri huo.
TUONANE TENA PANAPO MAJALIWA:- Kapulya/dada mkuu.
 

4 comments:

Daniel Hhary said...

hongera wahehe kwa kuendelea kudumisha mila na utamaduni wenu na kuacha kufuata utamaduni wa kizungu ambao hatujui chanzo chake ni wap, malengo yake ni yap?

Yasinta Ngonyani said...

Daniel Ahsante sana kwa mchango wako... kwa kweli inafurahisha kuona baadhi ya makabila wanazidi kudumisha utamaduni, mila na desturi.

Nicky Mwangoka said...

Mila na desturi zetu lazima ziendelezwe kwa vizazi vya sasa na baadae

Yasinta Ngonyani said...

Kaka Nicy! hivyo unawaza wewe na mimi je wengine wote wanawaza hivyo? ingekuwa hivyo basi ingekuwa hazifi....