Wednesday, June 15, 2011

NDOA YA MALAIKA HAIJAWAHI KUWEPO DUNIANI!!!

Kama kawaida leo ni jumatano ambayo ni siku ya kile KIPENGELE CHETU CHA MARUDIO haya karibuni tujumuike nami!!!!!





Wakati mwingine misukosuko ya ndoa huwaliza wanawake,


lakini hizo zote ni changamoto !


Kuna kudanganyana kwingi kuhusu ndoa pale mtu anaposhindwa kuwa mwangalifu sana kwa kauli za wengine walio kwenye ndoa. Hii hutokana na ukweli kwamba kuna kujumuisha kwingi sana. Kuna wakati huwa tunasikia au kuambiwa kwamba ndoa ni sawa na jehenamu. Baadhi ya watu walio kwenye ndoa kuna wakati huzungumza kwa njia ambayo hutufanya tuamini kwamba kuoa au kuolewa ni jinai. Ndoa ni ujinga mtupu haina maana, mtu anaweza kusema. Wasemaji hawa wanaweza kuwa ni watu tunaowaamini sana kama wazazi wetu na wengine wa aina hiyo.
Baadhi ya watu badala ya kuponda na kubeza kuizungumzia kama kitu kizuri sana kisicho na doa wala chembe ya usumbufu. Inawezekena kabisa nasi tukawaamini wazungumzaji hao, hivyo kuamini kwamba, ndoa hazina usumbufu.
Inawezekana dhana hii ikaingizwa vichwani mwetu wakati tukiwa wadogo au hata tukiwa watu wazima. Hebu fikiria juu ya mtu ambaye anajisifu kwamba ndoa yake haina hata chembe ya mkwaruzo. Ambaye anaieleza ndoa yake kwa njia yenye kushawishi kuwa, kumbe ndoa zenye matatizo siyo ndoa bali kisirani kitupu. Kama nawe uko kwenye ndoa na ndoa hiyo ina matatizo hata madogo unaweza kudhani kwamba ulikosa kuoana na huyo mwenzako. Dhana hiyoinaweza kuchipuka kutokana na kauli kama hiyo inayoelezea ndoa kama kitu kisicho na mikwaruzo hata kidogo.
Kama usipokuwa mwangalifu unaweza kuacha kuchukua hatua za kujaribu kuondoa tofauti zilizo kwenye ndoa yenu. Utaacha kufanya hivyo kwa sababu mtu fulani atakuwa tayari ameingiza kichwani mwako uongo kwamba ndoa ni “asali” na “maziwa” matupu. Ni uongo kwa sababu hakuna ndoa isiyo na mikwaruzo.
Tunatakiwa kujua kwamba lengo la ndoa siyo kuepuka kukorofishana , hapana . Ukweli ni kwamba kukorofishana kunapotumiwa vema huweza kujenga uhusiano mzuri na imara sana. Kwa sababu kukorofishana hakuwezi kuepukika kwenye ndoa kunatakiwa kutumika kama shule na dawa ya kuimarisha ndoa.
Bila kukwaruzana kwenye ndoa zetu inaweza ikawa vigumu sana kwetu kubandua tabaka la uongo lililotufunika ambalo humfanya kila mmoja kati yetu kushindwa kuona na kumfahamu mwenzake katika tabia yake halisi.
Bila kukwaruzana, kila mmoja wetu atajidanganya kwamba anamfahamu mwenzake kama alivyo wakati siyo kweli. Tunapokwaruzana tunapata nafasi ya kufahamiana vizuri katika hali halisi.
Mwanamke mmoja maarufu aliwahi kuulizwa kama huwa anakwaruzana na mumewe. Alikiri kwamba huwa wanakwaruzana kwa kusema , “ndiyo tunakwaruzana, vinginevyo tungekuwa hatuna tofauti, na hapo bila shaka ndoa na maisha vingekuwa vimepooza sana”. Huo ndiyo ukweli wenyewe, kwamba bila kukwaruzana hatuwezi kufahamiana vema na kujua kwa undani tofauti kati yetu na wenzetu.
Inabidi tujue kwamba hakuna binadamu aliyekamili, yaani asiyekosea, kama ilivyo dunia yenyewe. Kwa hali hiyo hakuna ndoa ambayo haina makosa, kwa sababu ndoa ni binadamu hao ambao siyo kamili. Kwa hiyo, mtu anapotarajia kuwa au kuishi kwenye ndoa isiyo na kukwaruzana, ni sawa na mtu huyo kutarajia kukutana na binadamu ambaye ni kamili, yaani asiyekosea.
Kutarajia kuwa na ndoa ambayo haina kukwaruzana kunaelezwa kuwa ni chanzo kizuri sana kwa ndoa nyingi kulegelege au kuanguka kabisa. Mtu anapoingia kwenye ndoa akitarajia kwamba huko hatapambana na maudhi au kero za aina fulani, ni lazima ajue kwamba, hatadumu kwenye ndoa yake kwa sababu ndoa hiyo anayoitarajia haipo.
Mtu ambaye hakubali au angalau hataki kuelewa kwamba, ndoa ni lazima iwe na mikwaruzo anaweza kukabiliwa na tatizo lingine baya zaidi kwenye ndoa yake. Kwa kutokujua au kuepuka kukwaruzana, hawezi kuwa tayari kukubali kujadili migogoro ya kindoa ili kupata ufumbuzi. Hawezi kulikubali hilo kwa sababu haamini kwamba ndoa yenye kukwaruzana ni ndoa.
Wakati mwingine rafiki, ndugu au jamaa zetu hutusimulia jinsi ndoa zao zisivyo na kukwaruzana kama kwamba ni za malaika watupu. Bila kujua, huwa tunajikuta tumewaamini. Tunapowaamini huwa tunachukulia kukwaruzana kuliko kwenye ndoa zetu kama jambo au kitu ambacho hakikutakiwa kuwepo. Hapo hujikuta tukitamani kuondoka kwenye ndoa hizo kwa matarajio kwamba tunaweza kukutana na “malaika” ambao tutajenga nao ndoa zisizo na doa.
Hata pale ambapo tunasema wanandoa wanapendana sana, bado ndoa yao ni lazima itakuwa na kukwaruzana. Lakini wanachofanya hawa na ambacho huenda wengine hawafanyi ni kujadili tofauti hizo sawia na kuamua kuzisahau na hapo wote kukubali kujifunza kutokana na tofauti hizo.
Wale walio tayari kujadili tofauti zao sawia ndiyo ambao ndoa zao huwa na afya sana hadi wengine kushangaa kama siyo pamoja na kuona wivu. Wale wanaodhani ndoa ni mahali pa kila jambo kwenda kama mtu atakavyo, ndoa zao hupogoka vibaya na kufa kwa kishindo........

Makala hii nimeitoa katika Gazeti la Jitambue la hayati Munga Tehenan.

TUONANE TENA JUMATANO IJAYO PANAPO MAJALIWA!!!

10 comments:

emu-three said...

Kuna msemo nimeusikia jana kwenye mdahalo wa `Wanawake live' kwenye runinga zetu akisema kuwa `sufuria zinapowekwa pamoja hugongana na hata kukwanguana, sembuse sisi wanadamu...
Akiwa na maana kuwa lazima mnapokutana wawili hata kama mnapendana vipi, migongano na kutokuelewana kupo, ni swala ambalo halikwepeki kama binadamu.
Cha muhimu ni kukubali ukweli, kuwa na mawasiliano, na kujua misingi ya ndoa,...

Anonymous said...

Haya tena!. Ndoa ninzuri sana,na inapotokea ukabahatika kuwa katika ndoa shukuru mungu wako.Lamuhimu ninalo liona hapa katika mada hii,usumbufu,amajambo lolote litakalo leta mtafaruku wowote ndani ya ndoa,mimi naita ndo, ndoa yenyewe.ndoa nikati ya wawili,pamoja na wapambe,wazazi.ndugu jamaa na marafiki,mwisho wa yote ni wewe namkeo au wewe na mumeo ndiyo mtakuwa wawili chumbani mmenuniana,na wale wote walio toa ushauri watakuwa makwao,hakuna nafasi yakusema au kuliza fulani alisema je vile!?ni wewe na mumeo/mkeo ndo mnajuwa ugumu na uzitto wa tatizo,na nyinyi ndo wenye uamuzi kusuka ama kunyowa.kuvumiliana nimuhimu,kulia pia ni muhimu,kusameheana ni muhimu kutukanana nimuhimu,na yote haya ndiyo ndoa yenyewe,bila kusahau lazima muyamalize nyie wenyewe,na kama mna watoto,wao ndo wanatakiwa kunufaika na kusameheana huko.kwa kumalizia mawili muhimu,mawasiliano (kuwasiliana kuzungumza kila linapo tokea jambo ni muhimu) na kujishusha(kumfahamu mwenzio kwa undani mapungufu yake unapo mfehemu mwenzi wako ni rahisi kuepusha zali na hutaonekana mjinga au umelishwa limbwata ) Kaka S.

Rachel Siwa said...

Asante da Yasinta kwa elimu hii,ndoa ni neno dogo lakini lenye mambo mengi sana.@ kaka wa mimi Kitururu mbona unaguna au unaogopa?.lakini wewe nakuaminia ila yule bibi unayetaka kumuoa duhh mwenzio nina hofu.

Goodman Manyanya Phiri said...

Ndoa ni shughuli. Ni kazi ngumu sana lakini yarahisishwa na nia pamoja na ile hiari yako ya kuowa au kuolewa.


Hapana, Mdogo Wangu, Yasinta: ndoa za malaika zafinyika kila kukicha. Mimi ni malaika kwa mke wangu; naye pia malaika kwangu. (Hii dhana kwamba malaika ni kiumbe kingine tena cha ajabu na sio binadamu ni dhana potofu hata kwa maandishi matakatifu).


Ukiwa umewoa au kuolewa kwa sababu za ubinafsi tu au vishawishi, utakipata cha mtema kuni; na utakuwa umefunga pingu na shetani kabisa, wala si malaika!

Yasinta Ngonyani said...

emu-3! nimefurahi sana hapo uliposema "Cha muhimu ni kukubali ukweli, kuwa na mawasiliano na kujua misingi ya ndoa" kwani hakika hili ni MUHIMU SANA HATA KWA WAANZAO MAPENZI BILA MAWASILIANO SIO PENZI.

Simon!vipi? mbona miguno inazidi ndugu wangu?

Kaka S. Si utani yaani umepatia haswa "Ndoa ninzuri sana,na inapotokea ukabahatika kuwa katika ndoa shukuru mungu wako" ni kweli kabisa.

Rachel! si unajua elimu hawaninyimani ni mwiko... Rachel afadhali wewe umemuuliza huyu kaka wako labda tutapata jibu kama ni mguno tu au kuogopa kumbi unakaribia kuwa wifi mwenzako bila kujua...LOL

Kaka mkubwa Phiri! Ulichosema ni kweli ndoa si lelemama... duh hapa pazuri kweli nanukuu "Hapana, Mdogo Wangu, Yasinta: ndoa za malaika zafinyika kila kukicha. Mimi ni malaika kwa mke wangu; naye pia malaika kwangu. (Hii dhana kwamba malaika ni kiumbe kingine tena cha ajabu na sio binadamu ni dhana potofu hata kwa maandishi matakatifu)" mwisho wa nukuu. Ahsante kwa hili.

ray njau said...

NDOA-N=[DOA]/NDOA+NA=[NDOANA]
----------------------------------
N=[NYUMBANI]
D=[DAIMA]
O=[OMBENI]
A=[AMANI]
----------------------------------------------------------------------
Kwa miongo mingi asasi ya ndoa na familia imeendelea kukabili changamoto nyingi na mwisho wa yote imekuwa ni mtengano au talaka.Ni ni hasa chimbuko la changamoto hizi na je mtengano na talaka ndiyo hitimisho maridhawa la sinema hii ya ndoa na familia?Kwa haraka jibu ni ndiyo.
Wakati hayo yakiendelea hali halisi imeedhihirisha kuwa mtenagano na talaka siyo jibu sahihi la changamoto hizo kwa kuwa hii ni sawa na kulaumu ulipoangukia na kusahau ulipojikwaa.
Kila mdau katika asasi hii muhimu kijamii ni lazima ajiweke katika wajibu na madaraka yanayohusika ili awe katika nafasi nzuri ya kukabiliana na changamoto endelevu kwa kuzingatia masharti na viwango husika.

Serina said...

Det här är precis vad jag behövde läsa idag. Jag var på vägen att vara tokig men nu inser att det inte är mitt fel. Tack! att du ta upp dessa ämne Yasinta.

Yasinta Ngonyani said...

Serina vart är du? Saknar dig. Tack för uppmutring!!

yanmaneee said...

adidas yeezy
nike shox for women
coach outlet store
nike vapormax
yeezy sneakers
golden goose
coach outlet
air max
moncler
cheap jordans

Unknown said...

n7z16i8p36 t5k78o3c41 s7j39y9b17 t0e47h8y79 z3j45y3v81 f7v78b1y48