unaikumbuka hii? ebu soma tena ni vizuri kukumbuka zilipendwa....karibu
Wiki iliyopita na wiki hii nimekumbuka sana nyumbani, nadhani ni kwa sababu wiki
iliyopita tarehe 17 ilikuwa ni tarehe ambao mama yangu alifariki na wiki hii
23/5 imetimia miezi miwili tangu Mdogo wangu alifariki. Kwa kweli nam-miss sana
mama yangu pia mdogo wangu.
Nakumbuka ilikuwa kila nikienda likizo,
nilikuwa natumia muda mwingi kuwa jikoni na mama yangu nikizungumza naye
simulizi za kale za enzi ya utoto wangu.
Ni simulizi ambazo kwa kweli
kila nizikumbukapo huwa natamani yale maisha yajirudie kwani kuna mengi ya
kufurahisha na ya kuhuzunisha ambayo kwangu mimi nimejifunza mengi
kwako.
Lakini lipo jambo moja ambalo nimelikumbuka, ambalo kwa kweli huwa
linanifikirisha sana. Jambo lenyewe ni kuhusiana na baadhi ya marafiki zangu
kule nyumbani.
Kusema kweli ule ukaribu niliokuwa nao na baadhi ya
marafiki zangu umepungua kiasi cha kukatisha tamaa.
Sababu kubwa ni
kutokana na kile walichodai kwa nimewatupa kutokana na kutowasaidia kupata
wachumba wa Kizungu. Yupo rafiki yangu mmoja mbaye yeye aliwahi kunitamkia wazi
kuwa mimi ni mbinafsi kwa kuwa ni mara nyingi ameniomba nimtafutie mchumba wa
Kizungu kwa kuwa ninaishi huku ughaibuni lakini nimeshindwa
kumtafutia.
Nakumbuka nilimweleza ukweli kuwa siwezi kumsaidia juu ya
jambo hilo kwa sababu liko nje ya uwezo wangu, lakini kutokana na labda tuite
ufinyu wa kufikiri, nilimpoteza rafiki huyu kwa sababu ya kushindwa kumtafutia
mchumba wa kizungu……..yaani kaaaazi kweli kweli.
Hata hivyo nilijiuliza
swali moja, kuwa hivi hakuna wanaume huko nyumbani mpaka mtu aamue kutafuta
mchumba wa Kizungu? Je ni mapenzi au ni Uzungu unaotafutwa hapo?
Lakini
kwa upande mwingine sikumshangaa sana kwa sababu kwa huko nyumbani ipo silka ya
baadhi ya watu ambao wanaamini kwamba kuoa au kuolewa na Mzungu ni jambo la
kujivunia sana. Huwa nimezoea kauli za baadhi ya watu kule nymbani kila niendapo
likizo wakisema, ‘siyo mwenzako yule, kaolewa na Mzungu’ .
Yaani mpaka
leo hii bado kuna baadhi ya watu wanaamini kuwa kuoa au kuolewa na mzungu ni
jambo la kifahari na la kujivunia. Kinachotafutwa sio mapenzi tena ni huo
uzungu..
Kuna baadhi ya watu wamefikia hatua ya kuamini kuwa sisi
waafrika ni duni na wenzetu weupe ni bora na waliokamilika.
Lakini
nadhani makosa hayo hayakuanza leo, yameanzia mbali sana. Kwani kizazi na kizazi
tumekuwa tukiaminishwa kuwa wazungu ni bora zaidi yetu sisi.
Kwa mfano,
mtu kufanya mambo yake kwa umakini na anayefuata muda huyo ataitwa ni mzungu, au
mtu asiyependa majungu, uzinzi, uasherati na umbeya naye ataitwa kuwa ni mzungu.
Nakumbuka wakati nikisoma kule nyumbani, ilikuwa kama kuna mwalimu ambaye ni
mwadilifu kwa wanafunzi na anayewajali, utawasikia wanafunzi wakisema, ‘yule
mwalimu ni mzungu’
Yaani kipimo cha kufanya mambo kwa uadilifu na
kuwajali wengine kimekuwa kikihusishwa na uzungu, mpaka imefikia mahali kila mtu
anatamani kuolewa au kuoa mzungu wakiamini kuwa hao wamekamilika.
Hata
huko makazini napo watu wanaochapa kazi kwa uadilifu wanafananishwa na wazungu.
Wakati mwingine huwa nacheka kwa sababu naamini hao wanaoamini kwamba mtu kuwa
mzungu anakuwa amekamilika ni wazi kwamba hawawafahamu watu hao.
Kwamba
kuwa mzungu ni kutokuwa na tabia mbaya, kama uvivu, udokozi, kutojali muda,
kusengenya, umbeya, wivu, au kijicho, uzinzi, uasherati, ushoga na tabia zote
mbaya tunazozijua hapa duniani, nikujidanganya bure.
Nasema kuamini hivyo
ni kujidanganya, kwa sababu kwa wale wanaoishi huku ughaibuni au wale wanaofanya
kazi na hawa wenzetu huko nyumbani, watakuwa ni mashahidi wangu.
Kama
mlikuwa hamjui ni kwamba hawa wenzetu nakubali kuwa wapo waadilifu na wenye
tabia nzuri, lakini pia wapo wenye tabia za ajabu kama uvivu, udokozi, kutojali
muda, kusengenya, umbeya, wivu, au kijicho, kutojiamini, uzinzi, uasherati,
ushoga na tabia zote mbaya tunazozijua hapa duniani.
Ule udhaifu tulio
nao pia wenzetu hawa wanao tena wenzetu hawa wamepitiliza. Ila kutokana na
kudanganywa na TV na hizo kauli za wazee wetu tumejikuta tukiamini kitu ambacho
hakipo.
Mie wakati mwingine huwa nashangaa pale ninapokutana na baaadhi
ya Watanzania wenzangu ambao wanaishi au wamewahi kuishi huku ughaibuni
wanapozungumza kwa kubana pua kama hawa wenzetu. Wanashindwa kujua kwamba ile ni
lafudhi ambayo inatokana na lugha yao. Ni kama pale unapokutana na Mmakonde,
Mngoni au Msukuma au Mpare anapoongea Kiswahili kwa lafudhi ya lugha
yao.
Mbona wenzetu kwa mfano Wanaijeria au Wakenya wanaongea kwa lafudhi
ya lugha zao. Ni rahisi sana kumtambua Mkenya au Mnaijeria kutokana na lafudhi
yake pale anapoongea Kiingereza, tofauti na sisi ambapo Tunajitahidi kubana pua
mpaka tunajisahau hata pale tunapoongea Kiswahili.
Na ndio maana kuna baadhi
ya wanawake huko nyumbani na hata huku ughaibuni wamefikia hatua sasa wanaukataa
uafrika na kuanza kujichubua kwa mikorogo ili kuutafuta weupe.
Kuna
wakati nilipokuwa huko nyumbani nilishangaa kuwaona baadhi ya wasichana ambao
nawajua kabisa rangi zao kuwa ni weusi kama mimi lakini wamekuwa weupe mpaka
wanatisha! Tabu yote hiyo ni ya nini?
Tumefikia hatua sasa kila jambo
linalofanywa na hawa wezetu tunaiga, na ndio sababu siku hizi tabia kama za
ushoga, usagaji na tabia nyingine chafu tunazozishuhudia huku zimetamalaki huko
nyumbani.
Sisi kama Watanzania tunazo tabia nzuri ambazo hawa wenzetu
wanazitamani sana tofauti na tunavyodhani. Kwa mfano, sisi ni kawaida mtu kuamka
na kupita nyumba mbili tatu na kuwajulia majirani zake hali, au kuingia nyumba
yoyote na kama akikuta chakula akala bila wasiwasi.
Kwa upande wa Misiba
au harusi watu wamekuwa wakichangiana na kusaidiana kwa hali na mali, yaani
tumekuwa na ushirikiano wa hali ya juu tofauti na wenzetu hawa.
Kuwa
mzungu haimaanishai kuwa mwadilifu wala kuwa na tabia nzuri, bali tabia nzuri
inatokana na tabia ya mtu na malezi kwa ujumla wake, hakuna mahusiano yaliyopo
kati ya uadilifu, tabia nzuri na uzungu. Nasisitiza kuwa hakuna kitu kama hicho,
ni kujidanganya bure.
Inashangaza kuona kwamba, badala ya kujivunia tabia
hizi nzuri tulizo nazo ambazo hata hivyo wenzetu wanazitamani, tunatamani za
kwao ambazo nyingi ni mbaya na zenye kuumiza.
Tubadilike………………